
Darren Bent akifunga bao kwa kichwa
Darren Bent alifunga bao dakika
za mwisho mwisho na kumhakikishia kocha wao Rene Meulensteen matokeo
muhimu wakati wa mechi kati ya Fulham na Manchester United iliyochezwa
katika uwanja wa Old Trafford.
Fulham licha ya kushikilia nafasi ya mwisho
kwenye msururu wa ligi kuu ya Premier ilitoka sare ya kufungana magoli
mawili kwa mawili na mabingwa watetezi Manchester United.Fulham ndio iliyokuwa ya kwanza kuona lango la Manchester United, katika kipindi cha kwanza kupitia kwa nahodha wake Steve Sidwell.
Hata hivyo wenyeji walijikakamua kipindi cha pili ambapo walimiliki mpira kwa asilimia kubwa kabla ya Robin Van Persie kusukuma kombora kali lililomuacha kipa wa Fulham kinywa wazi.
Dakika mbili baadaye Michael Carrick vile vile alivurumisha kombora lingine ambalo liliwaacha wachezaji wa Fulham wakishangaa.
Kutangulia sio kufika

Kocha wa Manchester United David Moyes
Kama wahenga walivyonena, usikate kanzu kabla ya mtoto kuzaliwa, uwanja wa Old Trafford ulitulia kama kaburi, pale mchezaji wa ziada wa Fulham Daren Bent, alipofunga bao kwa kichwa baada ya kipa wa Man United David De Gea kutema mkwaju wa Kieran Richardson.
Huzuni ilitanda katika uwanja wa Old Trafford baada ya vijana hao wa Moyes kupoteza alama mbili muhimu na hivyo kudidimiza matumaini ya United ya kuhifadhi kombe hilo au hata kumaliza katika nafasi ya kwanza nne.
United ilifanya mashambulio mengi na wakati wa mechi hiyo iliandikisha krosi 81, kiwango ambacho ndicho kubwa zaidi kuwahi kuandikishwa na klabu yoyote tangu mwaka wa 2006.
United ambayo kwa sasa inashikilia nafasi ya saba kwenye msururu wa ligi kuu ya Premier imepangiwa kutoana jasho na Arsenal siku ya Jumatano na kocha David Moyes atakuwa na kibarua kigumu kutuliza nyoyo za mashabiki wao.
No comments:
Post a Comment